Watu zaidi ya 453 waliokuwa wakishiriki sherehe za hija wamefariki kwenye mkanyagano uliotokea karibu na mji mtakatifu wa Kiislamu wa Mecca, maafisa nchini Saudi Arabia wamesema.
Idara ya ulinzi wa raia nchini humo imesema kupitia Twitter kwamba watu wengine 719 wamejeruhiwa katika kisa hicho kilichotokea mji wa Mina, takriban kilomita tano kutoka mji wa Mecca.Shughuli za uokoaji zinaendelea, idara hiyo imeongeza.
Mkanyagano huo umetokea siku ya kwanza ya sherehe za Eid al-Adha.
Idara ya ulinzi wa raia Saudi Arabia imesema maafisa 4,000 wametumwa eneo hilo kusaidia pamoja na wahudumu 200 wa huduma za dharura.
![]() |
| Mahujaji hukusanyika kurushia mnara mawe kama ishara ya kumrushia shetani mawe |
Maafa hayo yalitokea mahujaji takriban milioni mbili walipokuwa wakishiriki moja ya faida muhimu za mwisho katika ibada za hija.
Maandalizi ya ibada hizo za hija yalikuwa yamekumbwa na mkasa baada ya kreni kuanguka katika msikiti mkuu wa Mecca mwezi huu na kuua watu 109.
Hii si mara ya kwanza kwa mikasa kutokea wakati wa hija.
Mikasa mingine iliyotokea wakati wa kuhiji:
2006: Mahujaji 364 walifariki wakati wa kurushia mawe mnara unaoashiria shetani
1997: Mahujaji 343 walifariki na 1,500 kujeruhiwa kwenye mkasa wa moto
1994: 270 waliuawa katika mkanyagano
1990: Mahujaji 1,426 waliuawa katika mkanyagano njia za kupitia chini za kuelekea maeneo matakatifu
1987: Watu 400 walifariki maafisa wa serikali walipokabiliana na waandamanaji waliounga mkono Iran


Post a Comment Blogger Facebook